Serikali imesema kwamba imebaini kuwa baadhi ya wanasiasa na taasisi za kiraia wanahusika katika kuhamasisha vurugu zinazoendelea mjini Mtwara.
Akitoa kauli ya Serikali bungeni jana, kwa niaba ya Waziri Mkuu, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi alirejea kauli ya Rais Jakaya Kikwete kwamba Serikali itawasaka watu wote wanaohusika na vurugu hizo ndani na nje ya nchi bila kujali umaarufu na madaraka yao.
“Baadhi ya taasisi za kiraia na vyama vya siasa kwa masilahi yao binafsi yasiyo na upeo mpana, vinaweza kudhani kuunga mkono madai ya namna hii ni kuimarisha kukubalika kwao miongoni mwa jamii,” alisema Dk Nchimbi: “Tunawakumbusha msemo wa wahenga usemao ‘tamaa mbele, mauti nyuma’... Tunaapa kuwasaka waasisi wa vurugu ndani na nje ya Mtwara, ndani na nje ya nchi yetu.
Wote waliohusika kupanga, kushawishi, kuandaa na kutekeleza vurugu hizo hawataukwepa mkono wa sheria.”
Alisema Serikali inalaani vikali vurugu hizo akisema wanaozihamasisha “wataipasua nchi, watasababisha vifo vya maelfu ya watu, watajaza taifa vilema na majeruhi na hawatanufaika na matokeo haya mabaya.”